Thursday 2 November 2017

KAMANDA TANGA,WAKULYAMBA AKIZUNGUMZIA JINSI WALIVYOFANIKIWA KUMKAMATA MTUHUMIWA WA MAUAJI YA WAFANYABIASHARA WAWILI NYUMBA YA KULALA WAGENI JIJINI HAPO,,

Pichani ni kamanda wa polisi mkoani Tanga,Benedict Wakulyamba akiwaeleza waandishi wa habari (hawako pichani) jinsi walivyofanikiwa kumkamata mtuhumiwa wa mauaji ya wafanyabiashara wawili walikutwa wamekufa nyumba ya kulala wageni Bomai Inn jijini Tanga.

NA SOPHIA WAKATI,TANGA
JESHI la Polisi Mkoani Tanga.linamshikilia mfanyabiashara, Ismail Yahaya Muhaji (41) mkazi wa Bulwa Amani wilayani Muheza,Dar e salaam na Tunduma mkoani Songwe akituhumiwa kuhusika kwa Mauaji ya watu wawili.

Kamanda wa Polisi Mkoani Tanga,Benedict Wakuyamba amethibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo akisema, kuwa mtuhumiwa tayari yuko mikononi mwa Polisi kwa mahojiano ili kujua kiini cha mauaji hayo. 

Alisema, mtuhumiwa ambaye ana makazi yake huko Bulwa Amani Muheza, Dar es Salaam na Tunduma Mkoani Songwe anahusishwa na mauaji ya Septemba 25 mwaka huu wa 2017 jijini hapo.

Kamanda,Wakulymba alisema kwamba katika kipindi hicho kulitokea mauaji ya kutatanisha kwenye nyumba ya kulala wageni ya Bomai Inn iliyopo Jijini Tanga. 

Kutokana na tukio hilo jeshi la Polisi liliendelea na uchunguzi hadi kufanikiwa kumnasa mtuhumiwa huyo mkoani Mwanza ambaye anaendelea kushikiliwa kwa uchunguzi. 

Aidha Kamanda Wakulyamba alitanabaisha kwamba katika mahojiano mtuhumiwa amekiri kutenda tukio hilo la kusikitisha kwa Jamaa zake hao waliofariki dunia. 

Alisema mtuhumiwa (Muhaji) amekiri kuwapa kilevi kikali (Valium)  marehemu hao wawili kwa kutumiwa mwanya wa ukaribu nao katika biashara walizofanya. 

Hata hivyo alisema, mtuhumiwa huyo tayari ameshafikishwa Mahakamani huku upelelezi ikiendelea kujua kisa na chanzo cha mauaji hayo ya kikatili. 

Kamanda huyo wa jeshi la Polisi Mkoani Tanga alisema jeshi la Polisi litaendelea kuwakamata wahalifu na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria ili haki kuweza kutendeka na amani kuimarika.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment