Saturday, 25 December 2021

KAMANDA WA JESHI LA POLISI WA MKOA WA TANGA AKIADHIMISHA WIKI YA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA JIJINI TANGA

 






NA SOPHIA WAKATI,TANGA

KAMANDA wa Polisi Mkoani Tanga, Safia Jongo, amekemea vikali ukatili wa kijinsia na kisaikolojia, amewasihi Watanzania kuacha vitendo hivyo ambavyo vimekuwa vikileta sura mbaya kwa Taifa.

Kamanda Jongo ametoa ombi hilo juzi wakati alipotembelea Shule ya watoto wenye ulemavu Pongwe,kituo cha watoto yatima na gereza la Maweni vilivyopo  Halmashauri ya Jiji la Tanga.

Katika ziara yake hiyo, Jongo aliambatana na askari polisi wanawake 'Tanzania Police Women Network' dawati la jinsia,ustawi wa jamii na taasisi nyingine ambazo ni sehemu ya wadau wa haki za watoto.

Alisema kuwa ziara hiyo imekuja katika siku 16 za kupinga 
ukatili dhidi ya jinsia na watoto  ambayo huadhimishwa kimataifa na Tanzania kwa ujumla.

Alisema lengo kubwa la siku hizo ni kupambana na 
ukatili wa jinsia na watoto na kwamba mbali na shughuli ya uelimishaji jamii wameona umuhimu kuwatembelea watoto wenye ulemavu Pongwe.

Watoto hao waliotembelewa ni wale wenye uoni hafifu na ulemavu wa ngozi wakiwa miongoni mwa makundi yaliyoathirika sana na 
ukatili hata kufikia hatua ya kutengwa na kufichwa majumbani wakionekana kuwa
mkosi.

Kutokana na hali hiyo,Kamanda Jongo amewaasa watanzania kuacha vitendo vya 
ukatili wa aina zote kwa madai kuwa vinachafua nchi na amehimiza mshikamano kutokomeza suala hilo.

"Siku 16 huadhimishwa kimataifa na mkoa tukaona tuungane na wenzetu kimataifa na Tanzania katika kupambana na 
ukatili wa jinsia na
watoto"alisema.

Johgoakiwa katika ziara hiyo amewaeleza watoto hao wa shule ya walemavu Pongwe kuwa wanapaswa kuona kwamba wanazo nafasi za kuwa viongozi kwenye Taifa hili huku akiwasihi kuongeza bidii kwenye masomo yao.

"Kikubwa ni kuwa na bidii kwenye masomo mnaweza kuwa Rais,mawaziri na hata askari polisi,ni lazima muwe na ndoto za kuwa na maisha bora ya baadae na kuwa na familia"alisema kamanda Jongo.

Amelieleza kundi hilo la walemavu kwamba linategemewa na serikali huku akiisihi jamii kuwaangalia kwa uoni maalum watoto wenye ulemavu mbalimbali.

Aidha aliwaasa wazazi kutokukata tamaa juu ya watoto wenye ulemavu akiwasihi kuwapeleka shule ili kupata haki yao kwani kinyume chake ni
kitendo cha 
ukatili.

Amesema shule ya msingi Pongwe yenye watoto wenye ulemavu inazo nafasi kupokea watoto hao ambapo jamii inapaswa kuitumia huku akiongeza kuwa suala la mifarakano ya wazazi ni sehemu ya 
ukatili ambao mwisho wake hupatikana watoto wahalifu.

Katika ziara hiyo ya siku 16 kupinga 
ukatili jeshi la polisi na wadau wake wametembelea maeneo mbalimbali sanjari na kutoa vifaa mchanganyiko vilivyogharimu Tsh 4 million.

Diwani wa Kata ya Pongwe,Mbaraka Saad amelipongeza jeshi la polisi,akisema ujio wao umeleta faraja kwa watoto hao wenye ulemavu akiwasihi wadau wengine kuiga mfano huo.

Naye Afisa maendeleo jamii wa halmashauri ya Jiji la Tanga,Bertha Dama alisema lengo la kuwa na siku 16 za 
ukatili wa kijinsia ni kutoa elimu ya ufahamu kwa jamii ili kuelewa madhara na athari zinazotokana na ukatili wa kijinsia.

Alisema Jiji la Tanga linakabiliwa na changamoto ya 
ukatili wa kijinsia kuanzia ngazi ya familia ambapo wazazi wameacha wajibu wa kuwalinda na kulinda usalama wa watoto

Mwisho.

 

No comments:

Post a Comment