Tuesday 25 July 2017

ZIARA YA WAZIRI WA ARDHI,NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI,LUKUVI ILIKUWA HIVI MNAZI,,

 Pichani katikati ambaye amesimama na kushika karatasi na kipaza sauti mwanaume ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi akiwahutubia wana nchi wa Mnazi wilayani hapo mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea shamba hilo linalo ungani vijiji vitatu vya Mbaramo,Shaghayu tarafa ya Umba na Mnazi wilayani Lushoto,mkono wa kulia ni mbunge wa jimbo la Mlalo Rashid Shangazi na mkono wa kushoto ni mkuu wa wilaya hiyo January Rugangika.

NA SOPHIA WAKATI,LUSHOTO
SERIKALI imesema inakusudia kulifutia hati shamba la mkonge la Mnazi Sisal Estate lililopo katika kata ya Mnazi kwa kile kilichoelezwa mwekezaji kushindwa kufuata taratibu zilizopo ikiwemo sheria namba tano ya matumizi bora ya ardhi.
Hata hivyo,imesema haitakuwa tayari kumvumilia mwekezaji ambaye atatumia teknorojia ya zamani na kuwa kikwazo cha ajira kwa wananchi wake huku lengo likiwa kufikia adhima ya rais Dk.John Magufuli kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi alitoa kauri hiyo juzi wilayani hapo mara baada ya kufanya ziara ya kutembelea shamba hilo linalo ungani vijiji vitatu vya Mbaramo,Shaghayu tarafa ya Umba na Mnazi wilayani hapo.

Baada ya kufuatia wamiliki wa kampuni ya Le-Marsh Enterprises ya nchini Kenya, kushindwa kulipa kodi ya ardhi tangu wamilikishwe shamba hilo mwaka 1997 pamoja na kushindwa kuliendeleza kutoa ajira kwa wananchi. 


Waziri,Lukuvi amesema amejiridhisha mbali ya kupokea malalamiko mbalimbali ikiwemo barua ya wananchi atamwandikia taarifa Rais Dk.John Magufuli kuonesha dhamira ya serikali ya kulifutia hati shamba hilo ili liweze kurejeshwa mikononi mwa serikal baada ya mmiliki wake kushindwa kuendana na masharti ya mkataba wa shamba wa umiliki wao.

Shamba hilo linamilikiwa na Wakenya wawili waliokuwa pamoja na watanzania wawili, lakini kwa mujibu wa waziri alisema kwamba watamshawishi Rais afute hati ya shamba hilo kutokana na kwamba wameshindwa kuliendeleza kwa kutumia mashine zile zile za mwaka 1951, lakini pia wameshindwa kulipa kodi ya serikal ya ardhi tangu mwaka 2012.

Alisema kuwa serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani iliunda kamati kila mkoa kufuatilia mashamba ambayo wawekezaji wameshindwa kuyaendeleza ambapo mkoani Tanga katika mashamba yaliyotembelewa mwaka jana rais aliyafutia mashamba matano katika wilaya za Korogwe na Muheza hivyo kuna uwezekanomkubwa kwa shamba hilo kufutiwa.

Hata hivyo,Waziri alimuuliza mmiliki wa shamba hilo Lawrence Macharia kwamba amekuwa akipata kiasi cha shilingi ngapi kwa mwaka ambapo alimwambia waziri kwamba pamojana gharama zote wanazotoa hupata kiasi cha shilingi bilioni 1 kwa mwaka jambo ambalo lilimsikitisha Waziri kuona ni kwanini wameshindwa kulipa kodi ya ardhi ya serikali kwa kipindi chote hicho.

Lukuvi alisema kwamba wakati shamba hilo wakilimiliki mweaka 1997 kodi ya ardhi kwa mwaka ilikuwa ni sh. 200 ambapo ikapanda hadi sh 400 na sasa serikali inatoza kiasi cha sh. 1,000 kwa mwaka kama kodi ya ardhi kwa sheria namba 5 ya ardhi.

"Mwekezaji hatulichukui shamba hili kwa sababu wewe ni Mkenya, tutachukua hatua kwa mujibu wa sheria ya ardhi na matakwa ya kisheria ya kituo cha uwekezaji hapa nchini,tuliwapa mashamba haya ili mlete teklonojia mpya, mjenge viwanda kwa mazao yatokanayo na mkonge"alisema Lukuvi.

Waziri alisema kuwa lakini pia muajiri wafanyakazi mlipe kodi ya serikali lakini yote hayo hayafanywiki kwa mwekezaji wa kiwanda hicho huku wananchi wakikosa ajira na serikali kukosa mapato yake ya ardhi.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Lushoto,Kazimbaya Makwega, alimueleza waziri kwamba kwenye kikao cha Kamati ya Ushauri cha mkoa wa Tanga (RCC) kupitia mkuu wa mkoa wake Martine Shigela waliagiza mashamba ambayo wamiliki wanashindwa kuyaendeleza wasitishe shughuli mbalimbali katika mashamba hayo.

Mbali ya kikao hicho ziko hatua mbalimbali kama halmashauri zilifikiwa ikiwemo kumpatia mwekezaji notisi ya siku tisini ili kuweza kujirekebisha kujitokeza ikiwemo kulipa kodi ya ardhi ya shamba hilo,kitu ambacho hakutekeleza.

"Licha ya kupata maelekezo kumwaandikia barua kwa baada ya kupata maelekezo ya kikao cha RCC, lakini pia tuliwakamata wafanyakazi wa shamba hili wakihujumu miundombinu, walikuwa wanataka wang'oa njia ya reli, kesi ipo polisi," alisema mkureugenzi huyo baada ya mmiliki wa shamba hilo kumweleza waziri kwamba wameshindwa kuliendeleza baada ya kupata taarifa kwamba shamba hilo tayari limechukuliwa na serikali.

 Huku Diwani wa kata ya Mnazi,Zuberi Shechambo alipopewa nafasi ya kueleza alisema kwamba mwaka 2002 alikuwa mwenyekiti wa kijiji cha Mnazi mwekezaji huyo alitaka kung"oa korona hiyo kwa lengo la kuiuza  ambapo alimzuia na kupelekea kuwepo mpaka leo.

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Mlalo,Rashid Shangazi, alimpongeza rais pamoja na waziri huyo kutokana na jitihada wanazozifanya kuwasaidia wananchi na kwamba anayoimani kubwa kwamba shamba hilo serikali italichukua na hivyo kuondoa kero ya muda mrefu ya wananchi wanaozungukwa na shamba hilo kukosa maeneo ya ujenzi wa nyumba, mashamba pamoja na huduma za jamii.

Hata hivyo,waziri Lukuvi alitumia nafasi hiyo kwa kuwataka viongozi kuanzia ngazi ya vijiji kwa kushirikiana na wananchi kuendelea kuwa walinzi kulitunza shamba hilo mpaka pale serikal itakapo fikia muafaka na kulipangia matumizi bora ya ardhi.
Mwisho.
Hii ndio korona ya tangu mwaka 1937 ambayo ni chakavu ilikutwa ikitumiwa na kiwanda hicho.

No comments:

Post a Comment