Sunday 20 August 2017

WANACHAMA WA TIMU YA COASTAL UNION WAMEKUTANA LEO KUWEKA MKAKATI MADHUBUTI,,,

NA SOPHIA WAKATI,TANGA
KLABU ya Coastal Union yenye maskani yake Jijini Tanga, imezika tofauti walizokuwa nazo awali zilizosababisha timu hiyo ishuke kutoka Ligi kuu ya Tanzania Bara msimu wa mwaka 2014/ 2015, na sasa timu hiyo imeunda umoja wa viongozi utakaokuwa na lengo la kuirejesha Ligi Kuu msimu ujao.

Akizungumza LEO saa tano asubuhi kwenye mkutano wa wanachama uliofanyika makao makuu ya klabu hiyo barabara ya 11 Jijini hapa, Mwenyekiti wa kamati ya mashindano, Ahmed Hilal maarufu ‘Aurora’ alisema kutokana na kikao kilichofanyika katika hoteli ya Mkonge, kimezika tofauti hizo na sasa wapo pamoja.

Alisema miongoni mwa watu waliohudhuria mkutano huo uliorudisha umoja ni pamojana,Nassor Binslum ambaye ataisaidia tena klabu hiyo pamoja na watu wengine ili kuhakikisha timu hiyo itakayoshiriki Ligi Daraja la kwanza iweze kurejea Ligi Kuu.

“Kiukweli mkutano uliofanyika Mkonge Hoteli umezika tofauti zote ambazo zilijitokeza awali na tumeunda umoja ambao umewezesha timu yetu kusajili wachezaji watakaokuwa na uwezo wa kupanda daraja,Tunachotaka sasa watu wote wajali Coastal kwanza mambo mengine ya baadaye,” alisema Aurora.

Hata hivyo,Coastal iliteremka daraja baada ya viongozi kuhitafiliana na  Aurora akiwa Mwenyekiti aliyeipandisha daraja timu hiyo msimu wa 2011-2012 alijiuzulu wadhifa huo na baadaye timu kufanya uchaguzi uliomweka madarakani Dk. Ahmed Twaha ambaye aliishusha daraja akiwa na katibu wake Kassim El-Siagi na Akida Machai.

Mgogoro huo ulisababisha baadhi ya watu kwenda kujiunga na timu ya Mgambo JKT ambayo nayo ilishuka daraja hadi la kwanza huku wanachama wengine wakienda katika timu hiyo ambapo zote mwaka jana ziliposhiriki ligi daraja la kwanza hazikufanya vizuri.

“Tumesameheana kabisa na sasa tupo pamoja, tusianze kunyoosheana vidole na kufukua makaburi yaliyipita hatutafika tunapotaka kwenda lakini lazima mkumbuke mpira sasa ni fedha…Nawakumbusha pia lipeni ada zenu muwe na sauti kwa viongozi hawa,” alisema Aurora.

Makamu Mwenyekiti wa timu hiyo,Mohamed Musni, alisema kwamba hivi sasa uongozi wa klabu hiyo umepanga kuhakikisha inafanya vizuri katika Ligi daraja la kwanza itakayoanza mwezi ujao ili waweze kurejea kwa kishindo Ligi Kuu.

Nae Mjumbe wa kamati ya utendaji ya timu hiyo Abdallah Zuberi ‘Unenge’, aliwataka wanachama kuhakikisha wanaacha majungu ya kupeleka habari zitakazowarudisha kule walipotoka na badala yake wahubiri umoja kwa faida ya timu hiyo.

Kwa upande wake kaimu Katibu Mkuu,Nassoro Kibabedi, alitumia nafasi hiyo kwa kuwataka wanachama waisaidie timu hiyo katika kipindi hiki na kamwe wasibweteke wakiamini kwamba wafadhili watafanya kila kitu hivyo walipeada zao ili ziweze kuisaidia klabu hiyo.
Mwisho.

NA SOPHIA WAKATI,TANGA
TIMU ya soka ya Coasta Union ya Jijini hapa, itaanza mazoezi kesho (Jumanne) kwenye uwanja wa Mkwakwani kujiwinda na Ligi Daraja la Kwanza (FDL), inayotarajiwa kuanza mwezi ujao huku ikitangaza nyota wake wapya iliyowasajili msimu huu.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya timu hiyo,Ahmed Hilal maarufu ‘Aurora’, alisema kazi ya usajili haina rahisi kutokana na kwamba kabla hawakuwa na fedha hivyo baada ya kurudisha umoja wameweza kusajili wachezaji wadhoefu watakaowasaidia kupanda daraja msimu huu.

Aurora aliwataja baadhi ya wachezaji wapya kuwa ni pamoja na mchezaji wa zamani wa timu ya Taifa ‘Taiufa Stars’, Simba na Yanga Athumani Idd ‘Chuji’, Hussein Sharrif ‘Cassilas’, Salvatory Ntebe kutoka Ndanda FC, Ramadhani Hassain kutoka Mbeya City, Maulid Rajab ‘Mau’ African Sports, Hilal Juma Mtibwa, Ramadhani Mussa Pamba, Ibrahim Ndanda, Baraka Jafar na Omary Salum kutoka African Lyion.

Huku wachezaji wengine ni pamoja na mfungaji bora wa Ndondo Cup iliyomalizika hivi karibuni Jijini Dar es salaam Rashid Roshi, Exavery Emanuel, Rahim Aziz Afrikan Lyion, Sagaf  Kabaki, Bakari Mtwiku, Bakari Nondo, Said Jeilani na Abubakari Kinanda ‘Mapara’ kutoka malindi ya Zanzibar.

Katibu wa klabu hiyo,Nassor Kibabedi alisema mazoezi yataanza kesho kwenye uwanja wa Mkwakwani asubuhi kishajioni yatafanyika kwenye uwanja wa shule ya sekondari Galanos ambako mwalimu atakuwa Joseph Lazaro.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment