Sunday 14 January 2018

WANANCHI WA VIJIJI VYA KATA YA PANDE DARAJANI WAMUOMBA WAZIRI WA ARDHI KUINGILIA KATI ZOEZI LA UHAKIKI MAJINA YA WATU,,,



 Pichani ni baadhi ya wananchi  wa vijiji vilivyopo kata ya Pande Daraja, wilayani Muheza wameimba serikali kupitia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kuingilia kati 'sakata la ugawaji mashamba' la Kibaranga baada ya zoezi linaloendelea la uhakiki wa orodha ya majina ya watu watakaopewa ekari tatu kila mmoja, kubaini majina mengi kukosekana.

NA SOPHIA WAKATI,MUHEZA
WANANCHI wa vijiji vilivyopo kata ya Pande Daraja, wilayani Muheza wameimba serikali kupitia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi kuingilia kati 'sakata la ugawaji mashamba' la Kibaranga baada ya zoezi linaloendelea la uhakiki wa orodha ya majina ya watu watakaopewa ekari tatu kila mmoja, majina mengi kukosekana.

Wananchi hao wakizungumza juzi huku wakionekana kukosa imani na zoezi zima la uhakiki linaloendeshwa na viongozi wa halmashauri, walisema vitabu vitatu vya majina vinavyotumika kutambua majina ya wananchi wa vijiji hivyo, hailingani na majina yaliyobandikwa katika ubao wa matangazo uliopo katika ofisi za vijiji vyao.

Mkazi wa kijiji cha Kibaranga, SelemaniSaid alisema wamegundua majina yao kukosekana katika vitabu hivyo baada ya kuelezwa kwamba halmashauri imetumia utaratibu wa kuandikisha majina kwa vipindi vitatu tofauti na endapo umekosekana kwa sehemu moja, jina lako linaondolewa katika orodha ya watu watakaopata mashamba.

Alisema wanamshukuru Rais John Magufuli kulifutia hati shamba la Kibaranga Estate na kulirudisha kwa wananchi hatua ambayo wanampongeza, lakini suala la kuligawa kunakofanywa na viongozi wa wilaya wanaonekana kushindwa kusimamia zoezi hilo ambalo linaweza kusababisha vita ya mashamba miongoni mwao.

"Hii siyo haki kabisa tumesoma na kukulia hapa Kibaranga haki zetu zote za msingi zipo hapa, tunapokosa mashamba maana yake ni kwamba serikali imepanga lengo la kutufanya tuendelee kuwa masikini...Wazo la Rais (John Magufuli) kufuta hati na kulirejesha shamba kwa wananchi maana yake ni kwamba anatupa fursa ya kulima ili tupambane na umasikini," alisema Malaila.

Sophia Petro mkazi wa kijiji cha Kibaranga alisema kwamba miongoni mwa majina ambayo yamekosekana ni pamoja na wananchi ambao kwa miaka mingi walilivamia shamba hilo na kulima hivyo mpango wa kisheria wa kupatia eneo katika shamba hilo, kukosa majina yao ni wazi hawatakubali nguvu zao zipotee bure.

"Ndugu mwandishi unajua hii itakuwa ni vita ya mashamba kuna watu wamelima na kupanda mazao ya kudumu katika hilo shamba wanategemea kwamba baada ya serikali kufuta hati, kila mtu atapewa eneo ambalo tayari amelilima sasa jina lake kukosekana unadhani atakubali?", alisema Mhina.

Mwananchi mwingine,Tulo Saguti,(54) mkazi wa Kibaranga alisema kwamba suala jingine lililojitokeza katika zoezi hilo la uhakiki wa mjina ni kukosekana kwa majina ya vijana, wazee na akina mama waliondoka katika vijiji hivyo kwenda katika miji mingine kutafuta maisha, wakielezwa kwamba hawahusiki ilhali awali wakati wa kuandika majina waliandikisha lakini kwa sasa majina hayo hayapo.

Alisema wananchi hao wanayo haki ya msingi kabisa kupata maeneo ya kulima kwavile maisha yao yapo katika vijiji hivyo na kwamba hata kama hawapo kwasasa lakini wamekuwa wakishiriki michango mbalimbali ya maendeleo hivyo kupewa mashamba katika ugawaji huo, wanastahili.

"Kiukweli tunasikitika sana na hali hii, tunamuomba Waziri wa ardhi afute zoezi hili lianze upya kwa kuwa wilaya imeshindwa kusimamia watu wengi wanaoishi katika vijiji hivi majina yao hayamo katika orodha waliyokuja nayo kutoka wilayani...Sisi ni wenyeji wa vijiji hivi tumekulia kwenye mkonge wazazi wetu wamelilinda na kulitunza shamba hili kwanini tukose haki hii leo katika mgawanyo?", alihoji mzee Tullo.

Mwananchi mwingine Said Mawaila mkazi wa Darajani, alisema kwamba zoezi zima linapaswa kufutwa kwa vile hata hao ambao majina yao yametajwa katika orodha za vitabu hivyo, lakini limeingia katika mzozo wa kisheria kutokana na kukosewa 'spelingi' katika majina hayo.

Alitoa mfano kwamba mjomba wake jina lake limetajwa lakini halioani na vitambulisho alivyokwenda navyo ambapo jina lake yeye ni Augostino linavyosomeka katika vitambulisho vyake vyote kikiwemo cha mpiga kura, lakini katika orodha iliyokuja na wataalamu jina lake limekosewa limeandikwa 'Agostine'.

"Sasa ametakiwa kwenda kuapa mahakamani ili athibitishwe kama ni yeye, sasa kwa ninavyowajua wazee wa kijiji atawezaje kwenda huko mjini kuapa, kwanza hajui anzie wapi na afanyeje...Kiukweli ni vema Waziri akaingilia suala hili vinginevyo tutakosa haki zetu za msingi wa kumiliki ardhi iliyotafutwa na Rais wetu mpendwa," alisema Zuberi.

Pia alitumia nafasi hiyo kuishauri serikali kwa viongozi wa halmashauri kama wamepanga kuwapa wananchi hao ardhi ni vema katika wananchi ambao majina yao yamekosewa katika maandishi , wakapeleka watu wa mahakama kwenda kuwaapisha kuliko jukumu hilo kuliacha kwa wananchi hao ambao kimsingi hawajui wataanzia wapi.

Mwanamke mwingine Amina Rashid ambaye jina la mumewe Juma Rajab lilitajwa katika uhakiki huo lakini alipofika mbele ya wataalamu hao wa halmashauri aliwaeleza kwamba mumewe amefariki mwezi uliopita kwa ajali ya maji hivyo angependa yeye atambulike badala yake.

Lakini mwanamke huyo alitakiwa akaape mahakamani kwamba Juma amefariki na yeye ni mkewe jambo ambalo lilimtoa machozi mwanamke huyo ambaye baadaye alipozungumza na gazeti hili, alisema kwamba hana uwezo wa kwenda Muheza kuapa lakini pia hajui ataanzia wapi.

"Naambiwa hapa niende nikaape mahakamani kwanza sina hela, lakini pia sijui naanzia wapi? Huko pia siwatataka cheti cha kifo cha mume wangu haya nitakitoa wapi, wachukue tu hilo shamba maana siwezi kufanya lolote," alisema huku akilia.

Hata hivyo, wanawake wengi waliojitokeza katika zoezi hilo walitoa malalamiko yao kwamba utaratibu uliotumika haukuwa mzuri kwasababu kila kaya inapewa ekari mbili, hivyo wao kama wanawake hawahusiki na zoezi hilo kwavile wamewakilishwa na wanaume wao.

Alisema kwamba wao kama wapiga kura wakubwa inapofika uchaguzi wowote walikuwa na haki ya kupewa ardhi ili waweze kuzitumia katika kazi za kulima kwasababu kummilikisha mwanaume ni kumnyonga kwani anaweza kuachwa au mume kuoa mke mwingine na kumpa sehemu ya shamba hilo.

Akijibu malalamiko hayo,Mkurugenzi wa halmashauri ya Muheza,Luiza Mlelwa ambaye wakati mwandishi akiwa eneo la tukio alisema zoezi hilo ni  kuandikisha majina ya watu wanaopaswa kumilikishwa ardhi hiyo zoezi lililofayika katika vipindi vya awamu tatu tofauti kuanzia mwaka 2015, 2016 na 2017 ambako walishirikiana na watendaji wa vijiji husika.

Mlelwa alisema waliendesha zoezi hilo kwa awamu tatu kwa lengo la kudhibiti watu wasiohusika kuvamia na kujiingiza na kupata ardhi bila ya utaratibu ambao wameuweka ili kuhakikisha hakutokei malalamiko miongoni mwa wananchi kuhusu shamba hilo.

Kuhusu kukosekana kwa majina ya vijana na watu wengine wanaoishi nje ya vijiji hivyo lakini ni wenyeji wa maeneo hayo, alisema hawapaswi kupata mashamba hayo kwa vile huko wanaokoishi watumie fursa zinazopatikana kutoka na kwamba Tanzania ni moja na mtu unaouwezo wa kumiliki ardhi sehemu yoyote na kwamba mashamba hayo yapo kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wanaoishi kwa sasa.

Akizungumzia suala la malalamiko ya akina mama pamoja na kukosewa na maandishi ya majina, Mkurugenzi huyo alisema wameandaa dawati la kushughulikia kasoro mbalimbali kwa lengo la kupokea dosari hizo na kisha kuzifanyika kazi inagwa alieleza kwamba linapotokea hakuna budi mhusika kufauta sheria inavyosema.

"Hawa akina mama sheria zipo wazi anapoachwa kama wana mali wamezichuma pamoja anapokwenda mahakamani anapata haki yake, na hawa majina yao yamekosewa tumefungua dawati la kushughulikia kasoro mbalimbali za zoezi hili, waende huko ingawa watatakiwa kwenda mahakamani baadaye," alisema.

Hata hivyo,Shamba hilo lenye ukubwa wa hekta 5,328 lipo katika kata za Misozwe, Kicheba na Pande Darajani lilikuwa likiilikiwa na Mamlaka ya Mkonge Tanzania na baadaye lilibinafsishwa kwa kampuni ya Katani Limited na miaka mingi lilitelekezwa na wananchi wa vijiji vinavyopakana na shamba hilo walianza kuvamia kulima mahindi, mihogo na mazao mengine ya kudumu.

Mgawanyo wa shamba hilo, ambalo aliyekuwa mbunge wa jimbo la Muheza Herbert Mntangi, alikuwa mara nyingi akiiomba serikali kuwagawia wananchi ili waweze kulima ambapo mwaka jana Rais Magufuli alilifutia hati ya umiliki na sasa halmashauri inasimamia ugawaji huo ambao tayari umelalamikia kutokana na kasoro hizo.

Vijiji vitakavyo husika kupata ekari mbili kila kaya ni pamoja na Darajani na Upare vilivyopo kata ya Pande Darajani, Kwerubuye, Kicheba A na B kata ya Kicheba na vijiji vya Mwarimba, Manyoni na Misozwe vipo katika kata ya Misozwe kwa diwani Jestina Mntangi.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment